MKUU WA MKOA WA SONGWE AONGOZA KIKAO CHA BARAZA LA MADIWANI WILAYA YA MOMBA KUJADILI HOJA ZA CAG
Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mhe. Daniel Chongolo, ameongoza kikao maalum cha Baraza la Madiwani kilichofanyika leo tarehe 11 Juni, 2025 katika Halmashauri ya Wilaya ya Momba, kwa lengo la kujadili hoja zilizobainishwa katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Chongolo ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Momba kwa kupata Hati Safi, akieleza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya juhudi kubwa za kiutendaji na usimamizi mzuri wa rasilimali za umma.
“Niwapongeze Halmashauri ya Wilaya ya Momba kwa kupata Hati Safi. Sisi tuwapongeze kwa kazi kubwa mnayoifanya Halmashauri, lakini pia niwapongeze Mkaguzi wa Nje kwa sababu kupata Hati Safi kuna kazi kubwa ambayo imefanyika na kuwezesha kupatikana kwa hati hiyo. Mimi niwapongeze kwenye hilo,” alisema Mhe. Chongolo.
Aidha, Mhe. Chongolo ametoa rai kwa wataalamu wa halmashauri kujiepusha na kuwa chanzo cha hoja kwa kuzingatia maadili, weledi, na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Momba, Kamati za Ulinzi na Usalama za Mkoa na Halmashauri, wataalamu wa Halmashauri pamoja na Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Momba.
2 Nselewa Mkoani RD, 54180 Mlowo-Mbozi
Anuani ya Posta: P.O.BOX 23 SONGWE
Simu: 025 2580305
Simu ya Kiganjani: 025 2580305
Barua pepe: ras@songwe.go.tz
Hakimiliki©2020 Mkoa wa Songwe.Haki Zote Zimehifadhiwa.