Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mhe. Jabiri Makame leo tarehe 02 Februari 2026 ameongoza Maadhimisho ya Siku ya Sheria mkoani Songwe, ambapo ametumia fursa hiyo kuipongeza Mahakama Kuu ya Tanzania chini ya Jaji Mkuu Mhe. George Masaju pamoja na mahakimu wote wa Mkoa wa Songwe kwa kuungana na Mahakama Kuu ya Tanzania kuadhimisha Siku ya Mahakama Duniani, chini ya kauli mbiu “Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa.”
Akizungumza katika maadhimisho hayo, RC Makame amesema ili kuwepo ustawi na utawala bora ni lazima kuwe na mgawanyo wa majukumu na madaraka, akisisitiza kuwa Tanzania inajivunia muhimili wa kimahakama kwa kuendelea kutekeleza majukumu yake ipasavyo.
Ameeleza kuwa muhimili huu ni nguzo muhimu katika kuvutia uwekezaji kwani hujenga imani na uhakika wa usalama wa mitaji, sambamba na kuwa msingi wa kutatua changamoto za kisiasa kwa haki na usawa.
Aidha, amezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa, TAKUKURU, madalali wa mahakama pamoja na wadau wote kushirikiana kwa karibu na muhimili wa mahakama ili kuongeza ufanisi na kupunguza malalamiko mbalimbali yanayojitokeza katika utoaji wa haki. Amesema kila mdau ana wajibu wa kusaidia kuimarisha mifumo ya haki kwa maslahi mapana ya wananchi.
Katika hafla hiyo iliyohudhuriwa na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS – Songwe Chapter), watumishi wa mahakama, viongozi wa dini, machifu pamoja na wadau mbalimbali, RC Makame amesema Serikali ya Mkoa haita kuwa kikwazo katika kusaidia shughuli za kimahakama, bali itaendelea kushirikiana na kuongeza michango ili kuinua na kuboresha utoaji wa huduma za haki mkoani Songwe.
Kwa upande wake, Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Songwe, Mhe. Chami, amesema maendeleo ya teknolojia yamekuwa nguzo muhimu katika kurahisisha shughuli za kimahakama, akibainisha kuwa matumizi ya mifumo ya TEHAMA yameongeza ufanisi, uwazi na upatikanaji wa haki kwa wananchi.
2 Nselewa Mkoani RD, 54180 Mlowo-Mbozi
Anuani ya Posta: P.O.BOX 23 SONGWE
Simu: 025 2580305
Simu ya Kiganjani: 025 2580305
Barua pepe: ras@songwe.go.tz
Hakimiliki©2020 Mkoa wa Songwe.Haki Zote Zimehifadhiwa.